Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi ya Uganda (UPDF), Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ameagiza kukamatwa na kufungwa kwa Brigedia Jenerali Cyrus Besigye Bekunda.
Brig. Gen. Bekunda alikuwa kamanda wa brigedi ya ujenzi ya UPDF.
Yeye pamoja na maafisa wengine kadhaa wa jeshi wanachunguzwa kwa makosa ya rushwa.
Kupitia chapisho kwenye akaunti yake ya X (zamani Twitter), Gen. Muhoozi aliwatuhumu maafisa hao kwa kuchafua heshima ya jeshi na akasema adhabu yao itakuwa fundisho kwa wengine.
Alisema:
“Jana niliamuru kukamatwa kwa Brig. Bekunda Besigye pamoja na maafisa wengine kutoka brigedi ya ujenzi. Wamekumbatia rushwa, wamechafua, na kudharau kanuni takatifu ya UPDF kwamba tunaweza kujitegemea na kuwa na taaluma.”
Akaongeza:
“Walichukua pesa na kuzitumia vibaya! Adhabu yao iwe onyo kwa wengine.”
Kukamatwa kwa Brig. Gen. Bekunda kunafuatia kukamatwa kwa Kanali Godfrey Tukamwakira, aliyekuwa kamanda wa brigedi hiyo, kwa amri ya Jenerali Kainerugaba.




