Kamanda Mkuu wa Jeshi la Uganda, Jenerali Muhoozi Kainerugaba, ameomba msamaha kwa mjomba wake, Jenerali Salim Saleh, na kuahidi kwamba hatataja tena jina la Ujerumani mdomoni mwake.
Tangu mwishoni mwa wiki iliyopita, mvutano umeongezeka kati ya Uganda na Ujerumani baada ya jeshi la Uganda kumshutumu Balozi wa Ujerumani kwa kuunga mkono makundi yanayojitokeza kwa nia ya kupindua serikali ya Rais Yoweri Kaguta Museveni.
Jumapili, tarehe 25 Mei, UPDF ilitangaza kuwa imesitisha ushirikiano wa kijeshi na Ujerumani kutokana na mwenendo usiofaa wa balozi huyo.
Msemaji wa jeshi la Uganda, Kanali Chris Magezi, alisema ushirikiano wote kati ya UPDF na Ujerumani “utasalia kusitishwa hadi pale suala la Balozi [Mathias Schauer] ambaye anadaiwa kushirikiana na makundi ya kisiasa na ya kijeshi yanayopinga serikali litakapotatuliwa kikamilifu.”
Jenerali Muhoozi, kupitia ukurasa wake wa X, alishambulia balozi huyo na kusema shutuma hizo zinamhusu binafsi, si taifa la Ujerumani.
Hata hivyo, Jumatatu, Jenerali huyo alimkejeli balozi huyo kwa kuuliza ni kwa nini Ujerumani, nchi inayojulikana kwa watu warefu, ilimtuma mtu mfupi zaidi kuwa balozi wao nchini Uganda.
Alisema: “Kihistoria, Wajerumani wanajulikana kuwa watu warefu zaidi barani Ulaya baada ya Waholanzi wanaokunywa maziwa mengi kama sisi (Wahima, Watusi na Wadini wa Dinka). Basi kwa nini duniani wametuma balozi mfupi kabisa hapa?”
Ujerumani, kupitia msemaji wa Wizara ya Mambo ya Nje, ilisema shutuma dhidi ya balozi wao ni “aibu na hazina msingi wowote,” na wakazikataa vikali.
Licha ya hayo, UPDF inaendelea kumshutumu balozi huyo, huku baadhi ya wanadiplomasia wa Ulaya wakimweleza Gen. Saleh kuwa walitiwa wasiwasi na maneno ya Muhoozi.
Taarifa zinaonyesha kuwa Saleh, ambaye ni ndugu mdogo wa Rais Museveni, alimkemea Muhoozi na aliwahi kusema kwamba atamrekebisha mwenendo wake.
Kupitia ukurasa wake wa X, Gen. Kainerugaba aliomba msamaha kwa mjomba wake na kuahidi kutotaja tena jina la Ujerumani wala Wazungu.
Aliandika: “Kwa heshima kwa baba yetu mkubwa, Afande Saleh, sitawahi tena kutaja Ujerumani au Wazungu. Samahani Afande Saleh ikiwa nilikukosea heshima. Tafadhali nisamehe, Afande!”




