Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo (DRC) na Rwanda wamesaini mkataba wa amani mjini Washington tarehe 27 Juni 2025, chini ya usimamizi wa Marekani, huku mkataba mwingine kati ya Congo na AFC-M23 ukisubiriwa kusainiwa huko Doha. Hati ya Washington imetoa ratiba madhubuti ya kutekelezwa haraka, kama ilivyoripotiwa na vyombo vya habari vya Kimagharibi.
Mambo makuu yaliyokubaliwa ni:
Kwanza, kutakuwa na kipindi cha siku 15 cha maandalizi, kuchambua ukubwa wa tatizo, kutambua maeneo ya FDLR, na kushirikiana taarifa za kiusalama kati ya pande husika.
✅ Kufikia tarehe 27 Julai 2025, DRC na Rwanda lazima waanzishe mfumo wa uratibu wa pamoja, ambao utashirikiana na kamati ya ufuatiliaji ikijumuisha Umoja wa Afrika (AU), Marekani, na Qatar. Kikao cha kwanza lazima kifanyike kabla ya tarehe 11 Agosti.
✅ Katika eneo la operesheni, mambo mawili ya haraka yametajwa:
Kuvunjwa kwa kundi la waasi FDLR,
Kuondolewa kwa ngome za ulinzi za kijeshi za Rwanda.
Hatua hizi zimalizwe ndani ya miezi minne, kwa awamu tofauti.
✅ Kulingana na vyanzo vya RFI, operesheni za pamoja za kijeshi kati ya FARDC na RDF kuvunja FDLR zimekubalika, lakini uamuzi wa mwisho utatolewa kwa makubaliano ya serikali zote mbili.
✅ Kiuchumi, mkataba huu unajumuisha mpango wa kuunganisha uchumi wa kikanda, utakaozinduliwa tarehe 27 Septemba, wenye lengo la kuimarisha ushirikiano katika rasilimali, biashara, na uwekezaji wa mipakani.
Kuhusu suala la AFC/M23, wataalamu wanakubaliana kwamba ingawa mkataba wa Washington unaweza kuimarisha mazungumzo ya Doha kati ya DRC na AFC/M23, hauhakikishi mwisho wa mzozo, licha ya kuwepo kwa utulivu wa muda kwa sasa.




