Katika mkutano na Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa, Rais wa Marekani Donald Trump aliwasilisha makala ya habari iliyo na picha za mifuko ya miili ikizikwa, akidai kuwa ni wakulima weupe wa Afrika Kusini waliouawa kutokana na vurugu za kijamii, hata akafikia kuita tukio hilo kuwa ni mauaji ya halaiki.
Hata hivyo, video hiyo ilikuwa ni picha za Reuters kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, zilizopigwa mwezi Februari wakati wa mzozo wa Goma, zikionyesha wafanyakazi wa Msalaba Mwekundu wakishughulikia waathirika wa mgogoro wa kikanda .

Chapisho la blogu ambalo Trump alimwonyesha Ramaphosa wakati wa mkutano wao Ikulu ya White House lilichapishwa na American Thinker, jarida la mtandaoni la kihafidhina. Lilitumia picha za Kongo kuonyesha migogoro ya kijamii inayodaiwa kuwepo Afrika Kusini na Kongo, hasa wakati wa ushiriki wa kijeshi wa Afrika Kusini dhidi ya waasi wa M23.

Mwandishi wa Reuters Ali Katanty, aliyepiga picha hizo huko Goma, alieleza kusikitishwa na matumizi mabaya ya kazi yake, akisema: “Rais Trump alitumia picha zangu kutoka DRC kuashiria kwamba wakulima weupe wanauawa Afrika Kusini, jambo ambalo ni la kupotosha.”
Mahusiano kati ya Washington na Pretoria yamekuwa na mvutano tangu kuanza kwa utawala wa Trump. Wiki hii, Ramaphosa alitembelea Washington ili kuboresha uhusiano baada ya Trump kukosoa sheria za mageuzi ya ardhi za Afrika Kusini, ambazo Marekani inadai zinawalenga wakulima wachache weupe. Afrika Kusini inakanusha madai haya, ikisisitiza kuwa sheria hizo zinalenga kushughulikia tofauti za kihistoria za umiliki wa ardhi .





