Utafiti mpya uliochapishwa katika jarida la tiba la The Lancet umeonyesha kuwa uamuzi wa Donald Trump wa kupunguza misaada ya kigeni ya Marekani unaweza kusababisha vifo vya mapema vya watu zaidi ya milioni 14 kufikia mwaka 2030.
Utafiti huo unaonyesha kuwa asilimia moja ya tatu ya walioko hatarini kufa mapema ni watoto.
Katika mwezi wa Machi, Waziri wa Mambo ya Nje wa Marekani Marco Rubio alitangaza kuwa utawala wa Trump ulikuwa umesitisha asilimia zaidi ya 80 ya programu za shirika la USAID, ambalo hutoa msaada wa maendeleo duniani.
Davide Rasella, mwandishi mkuu wa ripoti hiyo alisema:
“Kwa mataifa maskini na ya kipato cha kati, hali hii ni kama janga la kimataifa au vita vikubwa vya silaha.”
Rasella, ambaye ni mtafiti katika Taasis ya Afya ya Ulimwengu ya Barcelona, aliongeza kuwa kukata misaada kunaweza kuwa na athari zisizotarajiwa au mbaya sana.
Ripoti hii imetolewa wakati viongozi wa dunia wanakutana mjini Seville, Uhispania, kwa mkutano mkubwa zaidi wa misaada wa Umoja wa Mataifa katika muongo mmoja uliopita.
Kwa mujibu wa takwimu kutoka nchi 133, watafiti walikadiria kuwa misaada ya USAID ilizuia vifo vya watu milioni 91 kati ya mwaka 2001 hadi 2021, kama ilivyoripotiwa na BBC.
Kama hali ya kupunguza misaada itaendelea, vifo zaidi ya milioni 14 vinaweza kutokea kufikia 2030, wakiwemo watoto zaidi ya milioni 4.5 walio chini ya miaka mitano, yaani watoto 700,000 kwa mwaka.




